Thursday, November 4, 2010

UKITAKA KUWA BORA KATIKA MAPENZI JIEPUSHE NA UVIVU, UCHAFU!

Mungu ni juu ya kila kitu kwenye Sayari ya Duniani na nyingine zote, kwani yeye ndiye muweza wa yote. Utukufu wake ndiyo unaotupa fursa tulizonazo, tunaishi kulingana na matakwa yake, kwahiyo sisi siyo lolote mbele yake. Tumshukuru na kumhimidi kwa kila hali.

Sasa tuzungumzie mapenzi, malove, katika sura ya kipekee kwa kuwa yanahitaji sana thamani ya hali ya juu. Yanaheshimika kupita kiasi kwasababu yenyewe ni sanaa ambayo kila mtu lazima atayapitia tu! Tunapenda na kupendwa, hivyo tupo mapenzini, ambaye hayumo basi pengine mambo yake siyo mazuri! Hata hivyo binadamu hatuko sawa, kila mtu anayo tafsiri yake anayoijua kuhusiana na mapenzi, ndiyo maana hatuachi kuelekezana.

Kila mmoja anapoingia katika uhusiano wa kimapenzi, moja kwa moja ndoto zake huwa ni kumfanya mwenzi wake kuwa wa kudumu. Atajiwekea malengo hata yasiyo tekelezeka ili mradi airidhishe nafsi yake. Hujawahi kuona mtu anapata mwenzi leo, kisha akaanza kupiga mahesabu ya kufunga nae ndoa? Ukweli ni kwamba wengi wetu tunapopata penzi jipya tunakuwa na matarajio mengi. Ni vizuri kuwa na matarajio na kujiwekea malengo ya kuyatimiza, lakini kosa kubwa ni kwamba huwa tunajisahau katikati ya safari.

Tunapenda sana kudumu na wenzi wetu tunaowapata, lakini ndoto hizo hugeuka za alinacha kama si kitendawili kwakuwa hatuwezi kujirekebisha ama kuficha makucha tuliyonayo. Matunda ya hali hiyo ni kuwa na kizazi chenye kujiwekea matarajio ya mashaka kila siku.

Pointi ya msingi hapa kama kweli tunataka kuwa na mapenzi ya kudumu ni kujua udhaifu wetu, angalia bado mapema, kutambua mambo ambayo ni sumu inayoweza kuua uhusiano wetu, ili tuzichukue kama changamoto, kisha tuzikabili na kuzishinda.

Tabia ambazo ni sumu katika mapenzi, ni hizi zinaweza kuubomoa uhusiano wako ndani ya muda mfupi. Muhimu ni kuzijua ili utambue namna ya kuziepuka. Unaweza kuziepuka kwasababu siyo maumbile, bali ni kujiendekeza tu! Ukiamini hakuna kitakachoshindikana, kwahiyo nakuasa uongozane na mimi mdogo mdogo ili upate jawabu la kutosha kuhusiana na mada hii;

UVIVU:
Hii ni sumu kali, lakini ni rahisi kuiepuka kama utaamua.Asili ya umbile la kila binadamu ndani yake kuna uvivu, na ni vizuri kutambua kuwa katika vitu ambavyo ni rahisi kumchefua mwenzi wako ni hili la uvivu.
Uvivu unaweza kuwa wa kujishughulisha katika mambo ya nyumbani ama utafutaji wa riziki, lakini baki ukijua kwamba tabia hiyo inakufanya ukalie kuti kavu kwenye uhusiano wako. Unashindwa kumsaidia mpenzi wako kazi ndogondogo, unaangalia nguo chafu haujitumi kuzifua, nyumba haitamaniki, hujiwezi kwa lolote, tabia yako hiyo inampa mwenzio tiketi ya kukuacha. Pointi hii inastahili kupigiwa mstari mwekundu na muhimu kwako ni kutambua ya kwamba uvivu utakupunguzia heshima na mvuto wako katika mapenzi.
Aidha kwa mwanamke ni janga ambalo mwanaume hatokawia kulikimbia, unadhani atawezaje kuvumilia kuwa na mtu ambae hajiwezi kwa lolote? Kujishughulisha hutaki! kuwajibika katika uwanja wa kuta nne ni ngoma nzito! atajiuliza; ni faida gani ya kuwa na wewe?

UCHAFU;
Tabia hii inaenda sambamba na uvivu, kwa kifupi ni kwamba uchafu ni matokeo ya uvivu. Mtu asiyejiweza kwa lolote hatomudu usafi, hivyo kutia sumu kwenye uhusiano wake.
Una tabia ya uvivu, kwahiyo ni mchafu.... unapaswa kutambua kuwa mwenzi wako anakerwa mno na tabia yako. Anza kwa kujichunguza mwenyewe ili kujua wewe ni mchafu kwa kiwango gani. Jawabu lako linaweza kukusaidia kwa kiasi cha kutosha, ikiwa utaamua kubadilika.
Unavaa nguo mpaka zinatoa harufu mbaya, ukiongea unatoa hewa chafu ya mdomo, kuoga kwa wasiwasi hadi mwili unanata, unashindwa kudhibiti jasho lako, mpaka unamsumbua mwenzako kwasababu ya kikwapa, kwa hali hiyo unategemea nini?

-Tuwe waangalifu sana katika maswala haya na tuyazingatie.....ukiachwa unaanza oh... mimi sina bahati, mara hivi mara vile, kumbe ni mambo haya tu!

No comments:

WATEMBELEAJI