Thursday, February 24, 2011

WATOTO YATIMA WATUNZWE KIFAMILIA ZAIDI....

WATOTO YATIMA WATUNZWE KATIKA MAZINGIRA YA KIFAMILIA ZAIDI, WAPEWE FURSA YA ELIMU NA USHAURI NASAHA. Wataalam wa maswala ya watoto na makuzi yao, wanabainisha kwamba; watoto yatima wanapaswa kusaidiwa kwa kubaki katika mazingira na maisha ya kifamilia zaidi. Kuhakikisha kwamba wanapata mahitaji yao msingi; fursa za masomo ili kuwajengea uwezo wa kujitegemea kwa siku za usoni, pamoja na kuwapatia ushauri nasaha na mambo ya kisaikolojia ili waweze kukabiliana na uhalisi wa maisha, badala ya kuishi katika ndoto, hali ambayo inaweza kuwafanya kukata tamaa na hivyo kukosa mwelekeo wa maisha.

Watoto wengi yatima ambao wameondokewa na wazazi na walezi wao, wanajikuta wakilelewa na Bibi na Babu zao au ndugu wa familia, hali hii inayoendelea kujenga uhusiano mwema kati ya watoto na jamii husika, kuliko tabia na mwelekeo wa watu wengi kutaka kuwapeleka watoto hawa katika vituo vya kutunza na kulelea watoto yatima.
Wazazi, kimsingi wanapaswa kuhakikisha kwamba wanaacha wosia kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watoto wao, kwani mara nyingi watoto yatima wamejikuta wakiporwa hata ule urithi kidogo walioachiwa na wazazi wao.

Wataalam hawa wanakiri kwamba; hali ngumu ya uchumi na ukata wa maisha kwa ujumla, unafanya ndugu wengi kutaka kuwapeleka watoto yatima kwenye vituo vya kutunza na kulea yatima, kutokana na uhalisi wa maisha yenyewe na changamoto wanazokabiliana nazo katika hija ya maisha yao ya kila siku. Walezi hawa pia wanapaswa kusaidiwa na wataalam wa masuala ya kisaikolojia ili waweze kuipokea na kukubali hali waliyo nayo kwaajili ya mafao ya watoto yatima.

Mara nyingi walezi wa watoto yatima, wengi wao hawapati ushauri wala msaada wa kijamii kama ambavyo ingepaswa kufanyika, hali inayowatendea hata watoto yatima wanapoishi katika mazingira kama haya. Walezi wa watoto yatima wahakikishe kwamba wanapewa ushauri wa kisaikolojia ili kupambana vyema na uhalisi wa maisha, kwa kuwahimiza kuwapeleka watoto yatima shuleni badala ya kuwaficha majumbani kwao, kisingizio cha ukata na hali ngumu ya maisha. Watoto wa maskini wakiwezeshwa katika elimu, wanaweza kufanya maajabu katika maisha yao ya hapo baadae.

-Jaribu nawe utaona tu!

No comments:

WATEMBELEAJI